Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Bunda (BUWSSA), siku ya tarehe 06/01/2025 ilitambulisha mradi wa maji kutoka Butiama hadi Nyamuswa, kwa wananchi wa Kata za Nyamuswa na Ketare, zilizopo Halmashauri ya Wilaya ya Bunda. BUWSSA ilitambulisha mradi huo kwenye mkutano wa hadhara ulioandaliwa na Mbunge wa Jimbo la Bunda Mh. Boniphace Getere, wakati alipokuwa akisikiliza na kutatua changamoto za wananchi wa Kata ya Nyamuswa.

Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa BUWSSA, Bi. Esther Gilyoma alisema Serikali ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Wizara ya maji inatekeleza mradi wa kusambaza maji kupitia chanzo cha maji ya ziwa Viktoria. “Utekelezaji wa mradi huo, unatarajia kuanza tarehe 01/02/2025 na kukamilika tarehe 30/01/2026, kwa gharama ya zaidi ya TShs Bilioni 8.3 ambazo zinafadhiliwa na Serikali kuu huku ukitekelezwa na Wakandarasi wawili ambao ni MOLI OIL MILLS pamoja na GAT ENGINEERING CO. LIMITED”. Alisema Bi. Gilyoma.

Mkurugenzi Mtendaji wa BUWSSA amesema, vijiji vitakavyo nufaika na mradi huo katika Halmashauri ya Wilaya ya Bunda ni vijiji vitano (5), ambavyo ni kijiji cha Bukama, Makongo A, Makongoro B, Nyamuswa na Tiring’ati.

Naye, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bunda Ndugu Stafa Nashoni, aliwashukuru na kuwapongeza BUWSSA katika usimamizi wa mradi huo na aliahidi kuwapa ushirikiano wa kutosha katika kuhakikisha wanatekeleza na kuukamilisha mradi huo kwa muda uliopangwa ili wananchi wa Nyamuswa na maeneo jirani waweze kunufaika na mradi huo.
Aidha Ndugu Nashoni alimpongeza na kumshukuru Mh. Mbunge kwa kuweza kusimamia na kuhakikisha mradi huo wa maji kutoka Ziwa Viktoria unaletwa katika Kata za Nyamuswa na maeneo Jirani.
Mradi wa majisafi kutoka Ziwa Victoria kupitia Wilaya ya Butiama hadi Nyamuswa unasimamiwa na Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Bunda (BUWSSA), chini ya Mkurugenzi Mtendaji wa BUWSSA Bi. Esther Gilyoma.



UPDATES : 23/01/2025
Mkataba wa utekelezaji wa Mradi wa Majisafi Nyamuswa umesainiwa rasmi tarehe 23/01/2025 katika ofisi za Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Bunda (BUWSSA).

UPDATES : 28/01/2025
Mnamo tarehe 28/01/2025, Naibu Waziri wa Maji Mhandisi Kundo Mathew amelieleza Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwamba mradi wa maji wa Nyamuswa unatarajiwa kuanza mwezi Februari 2025 na Mkandarasi ameshapatikana. Mhandisi Kundo alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Bunda Mhe. Boniphace Getere lililouliza ”Ni lini Serikali itatoa maji Ziwa Victoria kupitia mradi wa Mugango-Butiama-Kiabakari kuja Nyamuswa na kusambaa Jimbo zima la Bunda?’’
UPDATES: 26/04/2025
BI. ESTHER GILYOMA, ATOA SIKU 14 KWA MKANDARASI GAT ENGINEERING CO. LTD KUKAMILISHA UJENZI WA OFISI NDOGO NYAMUSWA
Mkurugenzi wa Mamlaka ya MajiSafi na Usafi wa Mazingira Bunda (BUWSSA) Bi. Esther Gilyoma, katika kuadhimisha sikukuu ya Muungano wa Tanzania amekagua maendeleo ya mradi wa maji wa Nyamuswa uliopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Bunda.
Bi.Gilyoma ametoa siku 14 ukamilishaji wa jengo la ofisi ndogo Nyamuswa uwe umekamilika kwa mkandarasi GAT ENGINEERING lengo likiwa kuruhusu kazi zingine za uchimbaji wa mitaro, ujenzi wa Matenki na ulazaji wa mabomba yenye urefu wa km 33 zianze mara moja.
Bi.Gilyoma amesema “Tunachohitaji ni kuona Wananchi wa Nyamuswa wanapata maji kufikia Mwezi wa kumi Mwaka huu, hatuna sababu ya kuchelewa na katika mradi unaotazamwa na serikali huu ni mmojawapo “
UPDATES – 11/08/2025

UPDATES – 22/08/2025

UPDATES – TAREHE 26/09/2025

UPDATES – TAREHE 02/10/2025
WATAALAM WA WIZARA YA MAJI WATEMBELEA NA KUKAGUA MIRADI INAYOTEKELEZWA NA BUWSSA
Wataalam kutoka Wizara ya Maji na Mfuko wa Taifa wa Maji wamefanya ziara ya kikazi kutembelea na kukagua utekelezaji wa miradi ya maji inayosimamiwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Bunda (BUWSSA). Miradi iliyotembelewa mnamo tarehe 02 Oktoba 2025 na kufanyiwa tathmini ni Mradi wa Majisafi Nyamuswa, Mradi wa Majitaka Butakale na Mradi wa Ubadilishaji wa Bomba Migungani – Kaswaka ikiwa ni miradi inayofadhiliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Katika ziara hiyo, Wataalam walipata fursa ya kujionea hatua mbalimbali za utekelezaji wa miradi, ubora wa vifaa vinavyotumika, pamoja na namna BUWSSA inavyosimamia matumizi ya rasilimali na utekelezaji kwa kuzingatia muda na viwango vilivyowekwa.
Lengo la kukagua utekelezaji wa miradi hiyo ni kuhakikisha viwango vya ubora vinazingatiwa, pamoja na kutoa ushauri wa kitaalam kwa ajili ya kuboresha utekelezaji wa miradi kwa viwango vinavyotakiwa.


Leave a Reply